Jumatano, 8 Julai 2015

KISHAZI KATIKA KISWAHILI



1.      KISHAZI
Ni aina ya tungo ambayo huwa na kitenzi ndani yake, kitenzi hicho kinaweza kikawa kinakamilisha maana au kisiwe kinajikamilisha kimaana. Kitenzi ambacho huwa kinakamilisha maana huwa ni kitenzi kikuu (T), na kile kisichokuwa kinatoa taarifa kamili huwa ni kitenzi kisaidizi (TS). Kwa mujibu huo tunapata aina mbili za kishazi yaani kishazi huru na kishazi tegemezi.
A.    Kishazi huru (K/Hr)
Aina hii ya kishazi huwa na tabia ya kutoa taarifa ambayo huwa ni kamili katika tungo, hubeba kitenzi kikuu au kishirikishi ndani yake. Kishazi hiki huwa hakihitaji maelezo ya ziada ili kukamilisha maana au taarifa kusudiwa na pia huweza kujitegemea kama sentensi kamili na huwa na muundo wa kiima na kiarifu.
Mfano; Mtoto / anacheza mpira
                  K                     A
            Mwanafunzi / anasoma kitabu
                  K                     A
            Mwanaume / anakufahamu
                  K                     A
           Mwanafunzi /. ni mpole
                  K                     A
B. Kishazi tegemezi (K/ Tg)
Aina hii ya kishazi huwa haitoi taarifa iliyokamili badala yake hutegemea kishazi huru ili kukamilisha taarifa iliyokusudiwa na msemaji. Kishazi hiki hutawaliwa na kitenzi kisaidizi. Kishazi tegemezi kwa upekee wake hakiwezi kutoa taarifa iliyokusudiwa. Vishazi tegemezi hushuka hadhi na kuwa na hadhi ya kikundi cha maneno (kirai).
Mfano;      Mtoto unayemjua
                  Mwanafunzi anayesoma
                  Mahali alipoingia
                  Mama alipomchapa
                  Kaka aliporudi
Vishazi hivyo hapo juu havitoi taarifa iliyokamili ila tunapoviweka pamoja na vishazi huru taarifa iliyokusudiwa hukamilika. Tazama hapa chini:-
Mfano;       Mtoto unayemjua ameondoka
                  Mwanafunzi anayesoma atafaulu
                  Mahali alipoingia ni pachafu
                  Mama alipomchapa aliondoka
                  Kaka aliporudi alinifurahisha
Sifa za kishazi tegemezi
                    i.            Hakikamilishi taarifa pasipokuwepo na kishazi huru
Mfano;       Mtoto anayecheza mpira ameumia
                  Mvulana aliyefaulu mtihani amefurahi
                  Mama alipomkaribisha aliingia ndani
                  ii.            Kinaweza kuondolewa katika tungo bila kuathiri taarifa kusudiwa.
Mfano;      mtoto aliyeugua amepona
                  Mtoto amepona
                  Mama uliyemsalimia pale ameondoka jana.
                  Mama ameondoka jana
                iii.            Hutambulishwa na vitambulishi vya urejeshi vinavyopachikwa katika vitenzi.
Mfano; Anayesoma, Alichookota, Uliokatika, Iliyoibiwa, Alipoingia n.k.
                iv.            Vilevile kashazi tegemezi hutambulishwa na viunganishi tegemezi kwamba, ili, ili kwamba, kwa sababu, mzizi wa amba na kiambishi cha masharti.
Mfano;       Mama alisema kwamba motto ameumia
                  Mvulana ambaye ni kaka yangu amerejea nyumbani
                  Akijua atanichapa
            Vishazi tegemezi vipo vya aina mbili kutokana na majukumu yake kimuundo
A.    Kishazi tegemezi kivumishi (bV)
Kishazi tegemezi kivumishi hufanya kazi ya kuvumisha nomino katika tungo.
      Mfano;            Baba anayenijali
                              Mbwa aliyepotea
                              Mwanafunzi aliyefariki
                              Uliyemuona pale
                              Aliyempenda sana

B.     Kishazi tegemezi kielezi (bE)
 Kishazi hiki hufanya kazi ya kueleza tendo katika tungo na hujitokeza kueleza dhima tofauti tofauti kama ifuatavyo:-
ü  Kueleza mahali tendo linapofanyika. Mfano; Alipoingia (mahali dhahiri), Alimochungulia (ndani ya kitu Fulani), Alikoelekea (mahali pasipo dhahiri)
ü  Kueleza wakati wa tendo. Mfano; Tulipotoka, Alipomchapa, Walipomsema n.k.
ü  Kueleza masharti katika tendo. Mfano; Akirudi, Angekuja, Angelimpiga, Angalijua n.k.
ü  Kueleza namna tendo linavyofanyika. Mfano; Alivyoimba, Walivyopendeza, Tulivyomsifu.
ü  Kueleza kasoro katika kukamilisha tendo. Mfano; Ingawa amesoma, Licha ya kufaulu, Japokua amependekezwa.
ü  Kueleza sababu ya kufanyika kwa tendo. Mfano; Kwa sababu alipendeza, Kwa kuwa hujafaulu, Kwa vile umenisomesha.

NGELI ZA NOMINO




    Ni namna ya kuweka majina katika makundi yanayofanana. Majina ya Kiswahili yanaweza kuwekwa katika makundi mbalimbali. Makundi hayo yamegawa na wanaisimu ya Kiswahili kwa kuzingatia maumbo ya alomofu za umoja na uwingi wa majina (kimofolojia) na kwa kuzingatia namna majina yanavyopatana na viambishi awali vya vitenzi (upatanisho wa kisarufi / kisintaksia).
1.      Kimofolojia: Katika kigezo hiki wanaisimu wameyapanga majina kulingana na alomofu za umoja na uwingi za majina hayo. Huu ni mtazamo mkongwe ambao uliofuatwa na wanasarufi wa kimapokeo wakiongozwa na Meinholf, Broomfield na Ashton mnamo miaka ya 1920 – 50. Uchambuzi ulikua kama ifuatavyo:-
1.      M-
2.      WA-
i). Majina ya viumbe vyenye uhai
ispokuwa mimea. Mfano; Mtoto – Watoto, Mzee – Wazee, Mkurya - Wakurya
ii) Majina yanayotokana na vitenzi
vinavyotaja watu. Mfano; Msomi – Wasomi, Mkulima – Wakulima, Mfanyakazi – Wafanyakazi.
3.     M-
4.      MI-
i). Majina ya mimea. Mfano; Mti – Miti, Mwembe, Miembe, Mpera – Mipera.
ii) Majina ya vitu yanayoanza na M- Mfano; Mto – Mito, Msumari – Misumari.
5.      KI-
6.      VI-
i). Majina ya vitu yanayoanza na ki- (umoja) na vi- (wingi). Mfano; Kiti – Viti, Kisu – Visu, Kikapu – Vikapu.
ii). Majina ya viumbe yanayoambishwa na ch- umoja na vy-uwingi. Mfano; Chura – Vyura, Chakula – Vyakula, Chuma – Vyuma.
7.      JI-
8.      MA-
i). Majina yanayoanza na ji- umoja na ma- uwingi. Mfano; Jicho – Macho, Jini – Majini, Jiwe – Mawe, Jina – Majina.
ii). Majina ya mkopo yenye ma- (wingi). Mfano; Bwana – Mabwana, Shati – Mashati.
iii). Majina yenye kueleza dhanna ya wingi japokuwa hayahesabiki. Maji, Majani, Maua, Maini.
9.      N-
i). Majina ambayo huanza na N inayofuatwa na konsonanti, ch-, d-,
g-, j-, z-, na y- katika umoja na wingi. Mfano; Nchi, Ndama, Ngoma, Njaa, Nzi, Nyasi.
ii). Majina yanayoanza na mb-, mv. Mfano; Mbwa, Mvi.
iii). Majina ya mkopo. Mfano; Taa, redio, Kompyuta, Kalamu.
10.  U-
11.  N-
i). Majina yote yanayoanza na U umoja na N-, mb (wingi). Mfano; Ubao – Mbao, Ulimi – Ndimi, Uso – Nyuso.
12.  U-
13.  MA-
i). Majina yote yanayoanza na uumoja na ma- wingi. Mfano; Uasi – Maasi, Uchweo – Machweo, Ugonjwa – Magonjwa.
14.  KU-
i). Majina yanayotokana na vitenzi yanayoanza na ku- (vitenzi-jina). Mfano; kucheza, Kulima, Kuimba, Kupenda.
15.  PA-

i). Huonesha mahali hasa. Mfano; Pale
16.  MU-
i). Huonesha mahali pa ndani. Mfano; Mule
17.  KU
i). Huonesha mahali pa mbali, pakubwa zaidi au popote. Mfano; Kule

UBORA WA KIGEZO CHA KIMOFOLOJIA
                   I.            Uwezekano wa kuzigawa nomino nyingi za Kiswahili ni mkubwa kwa kuwa nyingi zimegawanyika katika maumbo hayo ya umojha na uwingi.
                II.            Ni kigezo muhimu kwani kinajikita zaidi katika nomino na kivumishi chake peke yake hakigusi aina nyingine ya neno tofauti na kigeso cha kisintaksia ambacho hugusa hadi kitenzi.
             III.            Huwasaidia wanasarufi linganishi kuonesha uhusiano wa lugha za vikoa kimoja.

        UPUNGUFU WA KIGEZO HIKI.
                               I.            Kuna viambishi katika ngeli tofauti vinavyofanana. Mfano Kiambishi M- kinajitokeza katika ngeli ya 1 na 3 na MA- inajitokeza katika ngeli ya 8 na 13.
                            II.            Kuna nomino nyingine ambazo hazijidhihirishi katika umoja na uwingi. Mfano ngeli ya 8 na 9.
2.      Kigezo cha sintaksia /upatanisho wa kisarufi:
   Huu ni mtazamo wa kisasa wa uainishaji wa ngeli ambao umeyagawa majina katika makundi kulingana na upatanisho wa kisarufi kat ya jina na viambishi awali vilivyo katika vitenzi. Kwa mujibu wa mtazamo huu, majina yamepangwa katika makundi tisa ambayo ni:-
1.      A -WA
Mfano; Mtoto anacheza / Watoto wanacheza.
            Mzee analima / Wazee wanalima.
             Mwanafunzi anasoma / Wanafunzi wanasoma.
2.      U – I
Mfano; Mkufu umekatika / Mikufu imekatika.
             Mji umevamiwa / Miji imevamiwa.
             Mkaa umemwagika / Mikaa imemwagika.
3.      LI – YA
Mfano; Gogo limevunjika / Magogo yamevunjika.
             Gari limepotea / Magari yamepotea.
              Jiko limewaka / Majiko yamewaka
4.      KI – VI
Mfano;   Kiapo kimekiukwa / Viapo vimekiukwa.
               Kilima kimesawazishwa / Vilima vimesawazishwa.
               Kikongwe kimeuawa / Vikongwe vimeuawa.
5.      I – ZI
Mfano; Ng’ombe imechinjwa / Ng’ombe zimechinjwa.
             Nguo imechanika / Nguo zimechanika.
              Nchi imekosa amani / Nchi zimekosa amani.
6.      U – ZI
Mfano; Ubao umeandikika / Mbao zimeandikika.
             Ukuta umeanguka / Kuta zimeanguka.
             Uzi umetumika / Nyuzi zimetumika.
7.      U – YA
Mfano; Ugonjwa unatisha / Magonjwa yanatisha.
             Uasi umekithiri / Maasi yamekithiri.
8.      KU
Mfano; Kulima kunachosha.
             Kuimba kwake kunafurahisha.
           Kufurahi kwake kumemponya.
9.      PA – MU - KU
Mfano; Hapa pananuka.
             Humu mna nzi.
             Kule kumebomoka.
UBORA WA KIGEZO CHA KISINTAKSIA
n  Unajitosheleza kwa kuwa kila jina inakuwa na upatanishi wake katika kitenzi.
UPUNGUFU WA KIGEZO HIKI
I.                   Kuna viambishi vinavyojirudia. Mfano, U- kimejitokeza katika ngeli ya 2, 6 na 7.
II.                Huyaweka majina yenye maumbo tofauti katika ngeli moja.
III.             Kunaweza kuwa na utata katika upatanisho kwa baadhi ya majina kama “makala”
      Mfano; Makala yamechapishwa.
                  Makala imechapishwa.
Sentensi hizo zote zinatumika ila hatuna wingi wa makala katika Kiswahili